Friday 6 March 2015

APANDISHWA KIZIMBANI KWA TUHUMA ZA MADAWA YA KULEVYA


MKAZI wa Tarakea Wilayani Rombo mkoani Kilimanjaro Joseph Minja (29) amefikishwa katika mahakama ya wilaya ya Hai kwa tuhuma za kukutwa  na madawa ya kulevya aina ya bangi yenye thamani ya shilingi milioni 155.

Akisoma hati ya Mashtaka mahakani hapo, Mwendesha mashtaka wa polisi Roymax Membe amesema kuwa mtuhumiwa huyo alikamatwa na polisi katika eneo la Olmoloq Wilayani Siha akiwa anasafirisha kwenda nchi jirani ya Kenya.

Amesema mtuhumiwa alikamatwa na polisi mnamo Machi 3 mwaka  huu  majira ya saa 3 usiku  akiwa na bangi kiasi cha magunia kumi yenye jumla ya kilo 310 yenye thamani ya shilingi milioni   155

Amesema mtuhumiwa huyo ambaye pia ni dereva wa gari lililokutwa na bangi hiyo aina ya noah yenye namba za usajili T 470 BRC  inayofanya safari zake kutoka Moshi Mjini kuelekea Tarakea.

Hata hivyo, Membe ameieleza mahakama kuwa upelezi wa kesi hiyo bado haujakamilika   na kumwomba hakimu kutoruhusu dhamana kutokana na kosa alilotenda mtuhumiwa  kuwa na thamani ya zaidi ya shilingi milioni 10


Kutokana na ombi hilo la mwendesha mashitaka, Hakimu Agnes Mhina aliharisha kesi hiyo hadi Machi 19 mwaka huu itakapotajwa tena na mtuhumiwa amepelekwa gerezani mpaka hapo kesi itakapotajwa tena.

NA
Mwandishi wetu 

No comments:

Post a Comment