Friday 6 March 2015

DC ISOMENI KATIBA PENDEKEZWA KWANZA



Wananchi wilayani hai mkoani Kilimanajaro wametakiwa kuisoma na kuielewa katiba pendekezwa na hatimaye kuipigia kura ili kupata katiba mpya yenye kukidhi matakwa ya wananchi.

Hayo yamesemwa hii leo na mkuu wa wilaya mshikizi Novatus Makunga ambaye pia ni muu wa wilaya ya Moshi wakati wa uzinduzi wa katiba pendekezwa  uzinduzi ambao umehudhuriwa na viongozi wa serikali na taasisi mbali mbali zisizo za kiserikali.

Makunga amesema kuwa ni vyema wananchi wakatumia muda wao kuzisoma nakala za katiba pendekezwa zitakazotolewa katika maeneo yao na kuepukana na watu wanaoizungumzia katiba hiyo  pendekezwa bila ya kuwa na uelewa wa kile kilichoandikwa.

Awali akimkaribisha mkuu wa wilaya mshikizi, mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya ya Hai Melkizedeck Humbe amesema kuwa nakala hizo zitagawiwa katika kata, vijiji, zahanati, hospitali, vyuo na taasisi mbali mbali bila kusahau vijiwe mbali mbali vilivyopo wilayani hapa huku pia akimtaka kila mwananchi kuisoma katiba hiyo pendekezwa.

Naye mwenyekiti wa baraza la madiwani wa Hai Clement Kwayu amesema kuwa mwananchi ndiye mwenye maamuzi ya mwisho ambapo maamuzi hayo yatatolewa katika kura ya maoni ambapo kila mwananchi atapata fursa ya kushiriki kuipigia kura.

Kwa upande wake afisa habari wa wilaya ya Hai bi. Rizik Lesuya amesema kuwa wananchi watapata kuielewa katiba pendekezwa hasa ukizingatia halmashauri ya Hai inamiliki kituo cha redio Boma hai Fm ambacho kitafanya kazi ya kuuelimisha umma juu ya katiba pendekezwa kupitia vipindi vyake.

NA
Edwine Lamtey 0758-129821


No comments:

Post a Comment